Tuesday 1 April 2014

WAKATI VITA YA UJANGILI DHIDI YA TEMBO IKIENDELEA WATU 6 WANASWA NA MENO YA TEMBO

WATU sita wanaodhaniwa kuwa ni majangili wamekamatwa na meno ya tembo 53 yenye kilo 169.7, wakiwa na silaha aina ya SMG yenye magazine tatu kwenye Kijiji cha Kiomboi, wilayani Manyoni, mkoani Singida .
 Aidha, jumla ya tembo 26 wameuawa na majangili kwenye mapori ya akiba ya Rungwa na Kizigo yaliyopo wilayani humo.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, aliyasema hayo jana alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini hapa.
 Alisema kuwa majangili hao walikamatwa juzi majira ya saa 6:00 usiku na kikosi kazi maalumu cha kukabiliana na ujangili Kanda ya Kati – Manyoni ambapo wanashikiliwa kwenye Kituo cha Polisi Manyoni.

 “Msako zaidi unaendelea ili kuwakamata watu wote waliohusika na mtandao wa mauaji ya tembo hao 26 na Serikali inawaomba wananchi wenye taarifa kuhusu uhalifu huo wasisite kutoa ushirikiano kwa askari wa wanyamapori, Jeshi la Polisi na vyombo vingine vya ulinzi na usalama.” alisema  Nyalandu. 
Hata hivyo hakuwa tayari kuyataja majina ya watuhumiwa hao wa ujangili kwa madai kuwa hatua hiyo inaweza kukwamisha jitihada za kuwakamata majangili wengine. 
“Hawa tunaowashikilia inawezekana ni wabebaji tu, hawa watu huwa wana mitandao mipana sasa tunaendelea kusaka wenzao wakiwemo wale wanaowatuma na wasafirisha hivyo naomba nisitaje majina yao kwa sasa kuepusha hao wengine kutoroka,” alisema Nyalandu.
Katika hatua nyingine, Waziri Nyalandu amepuuzia tuhuma zilizoelekezwa kwake kuwa ameuza Hifadhi ya Taifa ya Katavi na inatarajiwa kukabidhiwa kwa wawekezaji kutoka nchini Afrika Kusini.
Alisema kuwa taarifa hizo hazina ukweli hata chembe kwani wizara yake haiwezi na wala haina mpango wa kuuza hifadhi yoyote wala maeneo yote yaliyo chini yake.
Waziri huyo wa Maliasili na Utalii alisema kuwa huenda huo ni mkakati wa majangili kutaka kubadili mwelekeo wa vita ya kukabiliana nao kwa kutumia baadhi ya waandishi wa habari kutoa habari za kupotosha umma hali itakayoifanya serikali kujikita kujibu tuhuma hizo za uongo hivyo kuwapa wao fursa ya kuendelea na ujangili.
 “Nadhani uandishi huu wa habari hauna thamani ya wino katika kalamu, kuweza kuandika uongo kama huo, Serikali ya Tanzania si kwamba tu haiuzi hifadhi ya aina yoyote lakini  hatuuzi pori.

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!