Friday 17 October 2014

SERIKALI YAFUTA MAFUNZO YA UALIMU NGAZI YA CHETI



============================== =====================


Serikali yafuta Mafunzo ya Ualimu ngazi ya Cheti

SERIKALI imefuta mafunzo ya ualimu ngazi ya cheti kuanzia mwaka huu ili kuboresha kiwango cha elimu nchini.




Tamko hilo limetolewa jana na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dkt.Shukuru Kawambwa wakati akizungumza na wanafunzi wa Chuo cha Ualimu Tabora, kilichoko Manispaa ya Tabora.
Alisema kuanzia mwaka huu, Serikali imeyafuta mafunzo hayo ikiwa ni mkakati maalumu wa kuboresha kiwango cha elimu ambapo walimu ambao wataajiri wakufundisha shule za msingi na sekondari, watatakiwa kuwa na elimu ya kiwango cha diploma na kuendelea.

Aliongeza kuwa, kuanzia sasa Wizara yake inataka kusimamia ubora wa elimu na walimu ambao kuanzia mwaka huu, wale ambao wataajiriwa kufundisha katika shule za msingi na sekondari, lazima wawe na elimu ya kiwango cha diploma na wasiofikia kiwango hicho, watapewa fursa ya kujiendeleza bila tatizo.

"Walimu wa shule za msingi na sekondari na wahitimu wa kidato cha sita waliopata daraja la 1-3 na kuchaguliwa kujiunga na kozi maalumu ya ualimu ngazi ya cheti, watapelekwa vyuoni kupata masomo ya diploma katika vyuo maalumu vilivyoandaliwa.

"Ili kuhakikisha mpango huu unatekelezwa, Wizara inaandaa waraka maalumu wamaelekezo ambao utatumwa kwa Wakurugenzi wa Halmashauri zote nchini," alisema Dkt. Kawambwa.

Awali, akijibu swali la mwanafunzi wa chuo hicho aliyetaka kujua kwanini muda wakufanya mazoezi kwa vitendo (BTP) umepunguzwa na kuwa wiki tatu badala ya siku 60, Dkt. Kawambwa alisema utaratibu huo ni wadharura kutokana na uhaba wa fedha.

Alisema Serikali itajitahidi kurekebisha hali hiyo kadri hali ya kifedha itakavyoruhusu ambapo akizungumzia ombi la kuongezwa posho kutoka sh. 4,500 wanazolipwa sasa hadi sh.7,500 ambazo wanalipwa wanafunzi wa ngazi ya Shahada, aliahidi kulifanyia kazi suala hilo katika Bajeti ya Wizara.

"Nawaomba wanafunzi wote wa vyuo vya ualimu, kuhakikisha mnafaulu masomo yote mnayofundishwa chuoni ili muweze kuajiriwa serikalini vinginevyo mtakaa benchi," alisema.
Dkt.Kawambwa alisema wakati anaingia katika Wizara hiyo, alisema hataajiri walimu waliofeli, hivyo ataendelea na msimamo huo kwa nia njema, hivyo wanafunzi waliopo shuleni wanapaswa kufaulu masomo yao na ya ziada ili waweze kuajiriwa.

CHANZO: Majira

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!