Friday 17 April 2020

Muhimbili yashona vazi la watoa huduma kujikinga na Corona."


Hospitali ya Taifa Muhimbili imeshona vazi maalumu (coverall) ambalo ni sehemu ya mavazi ya watoa huduma (PPE) kuvaa ili kujikinga wakati wanatoa huduma kwa Watanzania na raia ya kigeni watakaobainika kuambukizwa ugonjwa wa Corona (COVID 19) hapa nchini.




Akizungumza na wanahabari leo, Mkurugenzi wa Huduma za Tiba, Hospitali ya Taifa Muhimbili Dkt. Hedwiga Swai amesema jitihada hizi ni katika kuunga mkono kauli ya Mh. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kuwa Tanzania, tunaweza na siyo kila kitu lazima kitoke nje kwani malighafi zilizotumika zote zinapatikana katika viwanda vilivyopo hapa nchini.
Amesema PPE zinazotoka nje ya nchi hugharimu fedha nyingi za Tanzania ambapo vazi moja tu ni kati ya TZS. 350,000 hadi TZS. 500,000 ikitegemea imenunuliwa nchi gani, ambapo lililoshonwa na Muhimbili limegharimu TZS. 30,000.
"Tumeamua kushona vazi hilo ambalo linakaribiana na viwango vya WHO na sisi kama watoa huduma tulioko msitari wa mbele kuwahudumia, tumeridhika kuwa vazi hili linakidhi viwango na mahitaji yetu hapa nchini" amesema Dkt. Swai
Amesema katika kukabiliana na changamoto ya kutokapatikana kwa urahisi mavazi haya, Hospitali ya Taifa Muhimbili ina wajibu wa kutoa mwelekeo, ubunifu wa namna ya kutoa huduma nchini na hii ni sehemu ya wajibu huo.
"Tunatoa wito kwamba sasa viwanda vya ushonaji vinaweza kuja kupata sampuli ya aina ya vazi na malighafi zinazotumika ili bidhaa hii iweze kuzalishwa kwa wingi na kupatikana kwa gharama nafuu zaidi", amesema Dkt. Swai
Amesema, MNH inaipongeza Serikali kwa jitihada inazofanya na hatua mbalimbali zinazochukuliwa katika kukabiliana na ugonjwa huu ambao umeingia nchini nasi tunaendelea kushirikiana katika mapambano hayo.

EATV.

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!