Monday 2 April 2018

Habari zaidi juu ya Mtanzania aliyeua mkewe nchini Uingereza

MAUAJI yametokea alfajiri ya Ijumaa Kuu nchini Uingereza, yakihusisha Watanzania wawili. Tukio hilo limethibitishwa na ndugu na wanafamilia waliopo nchini.


Katika tukio hilo lililotokea mjini Haringey kaskazini mwa London, Uingereza, kijana wa Kitanzania aliyetambulika kwa jina la Kema Mobango Salum (Belly), anadaiwa kumuua mkewe, Leyla Mtumwa, mzaliwa wa Arusha, katika tukio lililohusishwa na ugomvi wa kifamilia.
Mtuhumiwa aliyekuwa akiishi jijini Dar es Salaam, inadaiwa alikwenda Uingereza mwaka jana kuungana na mkewe jijini London kabla ya tukio hilo la Ijumaa.
Inadaiwa kuwa, wanandoa hao waligombana kabla ya mtoto wa kiume wa Leyla mwenye umri wa miaka 12 kuwaita polisi baada ya Belly kumshambulia mkewe na kitu chenye ncha kali.
Mapema taarifa zilizokuwa zimezagaa kwenye mitandao ya kijamii, zilidai kuwa Leyla, mwanafunzi wa zamani wa Shule ya Msingi Arusha alitoka na marafiki zake usiku na kurudi asubuhi na kukutana na mumewe aliyekuwa amekasirishwa na kitendo cha mkewe kutoka na kumuacha nyumbani mwenyewe.
Leyla alisindikizwa na rafiki yake ambaye hata hivyo aliamua kuondoka baada ya kuona ugomvi baina ya wanandoa hao umefikia hatua ya kutishiana. Inaaminika kuwa baada ya rafiki huyo wa kike wa Leyla kuondoka, ugomvi wa kurushiana maneno makali ulisababisha mauaji hayo.
Baba wa mtuhumiwa, Kasambula Kema ambaye sasa anaishi Nairobi, Kenya amethibitisha kuwepo kwa tukio hilo.
“Mtoto wangu alizaliwa 1983 na mara zote alikuwa mtu mwenye tabia ya ugomvi, nilikuwa nikimuonya kuhusu tabia yake ya hasira na ni wiki iliyopita tu nilizungumza naye kwa njia ya simu na nilitumia wakati huo kumkumbusha kuwa yuko nchi ya kigeni ambayo haiwezi kuvumilia ugomvi au kupigana,” amesema Kassambula katika ujumbe wake mfupi wa maneno katika simu ya kiganjani.
Mama mzazi wa marehemu, Hidaya Mtumwa amesema anataka mwanawe aje kuzikwa nchini na mjukuu wake aliyemtaja kwa jina mola la Tarizi (miaka 12) ambaye ndiye aliyetoa taarifa ya mauaji hayo Polisi, kuja kushuhudia kaburi la mama yake mzazi.
Hidaya aliyasema hayo nyumbani kwake Mtaa wa Kaloleni jijini Arusha ambako ndipo kuna msiba huo huku wakisubiri taratibu zifanyike nchini Uingereza za kuusafirisha mwili wa mwanawe kuletwa Tanzania.
Alisema jana mchana aliwasiliana na ndugu yake hakumtaja jina, anayeishi Uingereza ambaye anashughulikia taratibu za kusafirisha msiba huo.
“Mchana huu ndio polisi Uingereza walifanya uchunguzi wa awali kubaini mwanangu nini haswa kimemuua na kisha tunasubiri taratibu za kuletwa nchini kwa ajili ya mazishi yake,” alieleza mwanamama huyo.
Mmoja wa majirani aliyemlea Leyla akiwa mdogo, Mary Sama amesema anasikitika kwa msiba huo kwani alimlea akiwa mdogo jijini Nairobi wakati mama yake Hidaya akiwa anafanya shughuli za biashara.
Mdogo wa marehemu, Abdul Karim alisema amepokea kifo hicho kwa mshtuko kwani dada yake aliolewa na mtuhumiwa Mei mwaka jana, na Desemba mwaka huo, shemeji yake alikwenda kumtembelea dada yake London.
Taarifa zaidi zinasema Kema aliyesomea nchini Kenya katika Chuo Kikuu cha Nairobi, alishawahi kufunga ndoa mara tatu; moja Zanzibar wakati akifanya kazi Zantel na ya pili Dar es Salaam alipoajiriwa na Airtel.
Inadaiwa aliachana na wake hao kutokana na tabia yake ya ugomvi. Wakati taarifa zingine zinadai kuwa Leyla alimtumia Kema tiketi ili waungane na kuishi wote London, baba wa mtuhumiwa alidai mwanawe aliuza gari lake moja ili kujilipia ndege kwenda Uingereza.
Leyla ni binti wa Hidaya Mohammed, mfanyabiashara wa Arusha na alishawahi kupata umaarufu baada ya kuimbwa na mwanamuziki wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Kabasele Yampanya maarufu Pepe Kalle katika wimbo wake wa mwaka 1991, 'Hidaya!' Baba wa Belly, Kasambula Kema maarufu 'Skassy Kasambula,' alikuwa mwanamuziki nyota nchini kabla ya kuhamia Nairobi.
Mama yake Belly, Bishada aliwahi kuimbwa mwaka 1981 katika wimbo 'Bishada' uliorekodiwa na Bendi ya Super Matimila na baadaye katika wimbo 'Mama Belly,' wa Bendi ya Sambulumaa mwaka 1989.
Alipoulizwa kuhusu mauaji hayo, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk Susan Kolimba alisema serikali imeshamuagiza Balozi wa Tanzania nchini Uingereza kufuatilia ukweli wa taarifa hizo.
Dk Kolimba alisema serikali haiwezi kuzungumzia taarifa za mitandaoni hivyo wananchi wanatakiwa kusubiri ukweli wa taarifa hizo ambazo Ubalozi wa Tanzania nchini Uingereza umeshaagizwa kuzifuatilia.
Kwa mujibu wa mtandao wa Polisi wa Metropolitan (http://news.met.police.uk/news/murder-investigation), Polisi imeanza kufanya uchunguzi wa tukio la mauaji ya mwanamke katika mji wa Haringey.
Maofisa wa polisi walidai kuwa walipigiwa simu asubuhi saa moja Ijumaa Machi 30, mwaka huu kwa saa za Uingereza wakielezwa kuwepo kwa tukio lisilokuwa la kawaida katika nyumba yenye anuani Kirkstall Avenue, N17.
Polisi wakiambatana na maofisa wa huduma ya gari ya wagonjwa London walimkuta mwanamke mwenye umri wa miaka 36, akiwa na majeraha ya kuchomwa na kitu chenye ncha kali, hata hivyo juhudi za kutaka kuokoa maisha yake zilishindikana na muda mfupi baadaye alipoteza maisha akiwa eneo la tukio muda wa saa 2:11 asubuhi kwa saa za huko. Juhudi za kutafuta ndugu zake wa karibu zinafanyika.
Polisi walisema mtuhumiwa ambaye ana umri wa miaka 38, alikamatwa kwenye eneo la tukio na anashikiliwa kwenye Kituo cha Polisi cha London Kaskazini.
Habari hizi zimeandikwa na Matern Kayera, Angela Semaya na Veronica Mheta

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!