Friday 20 October 2017

yaliyojiri leo Mahakamani katika kesi ya Lulu kuhusu kesi mauaji ya bila kukusudia ya Steven Kanumba


Kati ya mashahidi watatu waliotakiwa kutoa ushahidi leo katika Mahakama ya Kanda Maalumu Dar es salaam kuhusiana na kesi ya kuuwa bila kukusudia inayomkabili muigizaji Elizabeth Michael 'Lulu, wawili wamefanikiwa kutoa ushahidi huku mmoja  akitakiwa kufika Siku ya Jumatatu kwa zoezi hilo.

Kati ya mashahidi wawili waliofanikiwa kutoa ushahidi siku ya leo kuhusiana na kesi hiyo ni pamoja na aliyekuwa Afisa upelelezi Ester Zephania  ambapo amesema aliagizwa na kiongozi wake wa kazi kwenda eneo la tukio, ambapo amesema alipofika hakumkuta mshtakiwa 'Lulu'

Ameongeza kwamba, alipofika nyumbani kwa marehemu Kanumba chumbani alichofanikiwa kukikuta ilikuwa ni chupa ya pombe, michirizi ya rangi nyeusi ukutani pamoja na mapanga mawili na kuongeza kuwa mtuhumiwa, (Lulu) alikuja kumpata baada ya masaa mawili.

Pamoja na hayo amesema kuwa siku moja baada ya kumkamata mtuhumiwa akiwa mikononi mwa polisi alipelekwa hospitali kwa kuwa alidai kwamba anajisikia vibaya.

Kwa upande wa shahidi mwingine ambaye alikuwa Daktari binafsi wa marehemu Kanumba (Dk Kageiya), amesema kwamba alipopigiwa simu kuhusiana na hali ya mteja wake alipofika aligundua kuwa tayari alikuwa amekwishafariki lakini alishindwa kuwaambia ndugu zake.

Mahakama bado itaendelea kusikiliza ushahidi  siku ya Jumatatu  Oktoba 23, chini ya Jaji Sam Rumanyika kutoka kwa shahidi namba tatu ambaye naye ni Afisa Upelelezi.

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!