Wednesday 25 January 2017

TRUMP KAZINI: Tayari Wasomali na Wakenya wameondolewa Marekani, Kenya imethibitisha


Haijapita wiki moja toka Donald Trump aapishwe kuwa Rais wa 45 wa Marekani na kukabidhiwa ofisi, leo BBC wameripoti kwamba Raia takriban 90 wa Somalia na wawili wa Kenya wameondolewa kutoka Marekani.


Serikali ya Kenya imethibitisha kwamba Rais wote hao wamewasili katika uwanja wa kimataifa wa Jomo Kenyatta Nairobi ambapo msemaji wa serikali ya Kenya Eric Kiraithe amesema raia hao wa Somalia watasafirishwa moja kwa moja hadi Mogadishu.
“Ni watu 90 kulingana na habari ambazo tulipewa, na wakati unaondolewa nchi fulani kurejeshwa kwenu, huwa unarejeshwa hadi kwenu,” kuhusu sababu iliyowafanya kuondolewa, Kiraithe amesema: “Inategemea sheria za nchi ambayo walikuwa wamehamia (Marekani),”
 Trump alisema Jumatano itakuwa siku muhimu kwa usalama wa Marekani ambapo anatarajiwa kuweka masharti makali kwa raia wa mataifa saba ya Mashariki ya Kati na Afrika yenye idadi kubwa ya Waislamu wanaotafuta vibali vya kwenda Marekani.
Nchi hizo ni Syria, Iraq, Iran, Libya, Somalia, Sudan na Yemen ambapo kama unakumbuka wakati wa kampeni yake ya urais, Donald Trump aliahidi kufanyia mageuzi suala la uhamiaji Marekani.
Aligusia ujenzi wa ukuta kati ya Mexico na Marekani kuzuia wahamiaji haramu na kuwapiga marufuku Waislamu kuingia katika taifa hilo kama sehemu ya vita dhidi ya ugaidi lakini baadae alibadili msimamo kidogo na kufafanua kwamba watakachofanyiwa Waislamu ni kufanyiwa ukaguzi mkali kabla ya kuruhusiwa kuingia Marekani.
Trump anatarajiwa kufika katika wizara ya usalama wa ndani baadaye leo na anatarajiwa kusaini maagizo hayo ya kuimarisha usalama katika mpaka wa Mexico na taifa lake na baadae wiki hii taarifa zinaashiria atawajibikia ahadi yake ya kupunguza idadi ya wakimbizi wanaoingia Marekani.
Na hiyo ni hadi pale ukaguzi mkali utakapoanzishwa na kuzuia raia wa mataifa saba ya Afrika na kutoka eneo la Mashariki ya Kati yote yalio na idadi kubwa ya waumini wa Kiislamu.
Ubaguzi wa kidini unapigwa marufuku kwa mujibu wa katiba ya Marekani lakini inadhaniwa utawala wa Trump utaidhinisha marufuku hiyo kwa misingi kwamba ni hatua za dharura kukabiliana na tishio lililopo la ugaidi.

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!