Wednesday 6 January 2016

MAHAKAMA YAPIGA STOP BOMOA BOMOA, ZAIDI YA NYUMBA 15 000 ZAWEKEWA X


Wakati Mahakama Kuu ya Tanzania, Kitengo cha Ardhi ikiwa imesitisha bomoabomoa ya nyumba zilizoko mabondeni katika Manispaa ya Kinondoni hadi hapo kesi ya msingi iliyofunguliwa na Mbunge wa jimbo hilo, Maulid Mtulia na wakazi wengine itakaposikilizwa, zaidi ya nyumba 15,000 zinatarajiwa kubomolewa jijini hapa.

Bomoabomoa hiyo iliyoanza Desemba 17 mwaka jana, ilizikumba nyumba zaidi ya 300 katika Bonde la Mkwajuni wilaya ya Kinondoni, na ilianza tena kwa kwa kasi baada ya kusitishwa kwa siku 14 kupisha wananchi kujiandaa kwa kubomoa zaidi ya nyumba 300.
Kwa mujibu wa Ofisa Mazingira Mwandamizi Mkuu wa Baraza la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira, Arnold Kisiraga, nyumba zaidi ya 15,000 zimeshawekwa alama ya X hadi jana, wakati zaidi ya nyumba 600 zikiwa zimeshabomolewa.
 “Tumeanza na kasi kubwa tuna Tingatinga tano, tumebomoa maeneo la Bonde la Mkwajuni eneo lililokuwa limebaki na kata ya Hananasif kuelekea daraja la Salender na kesho (leo) tunatarajia kumalizia Salender,” alisema.
Kuhusu nyumba zilizowekwa alama ya X, Kisiraga alisema kazi hiyo iliendelea jana katika maeneo ya Buguruni kwa Mnyamani, Vingunguti na Tabata Segerea.
“Nyumba zilizowekwa X leo (jana)  ni zaidi ya 5,000 na hadi jana (juzi) tulikuwa tumeshafikia zaidi ya nyumba 10,000 kwa maana hiyo zaidi ya nyumba 15,000 zinatarajiwa kubomolewa,” alisema.
Aliongeza kuwa, uwekaji wa X utaendelea leo katika maeneo ambayo wananchi wamejenga mabondeni lengo likuwa ni kusafisha Mto Msimbazi wote.
CHANGAMOTO
Kisiraga alisema changamoto walioyokumbana nayo jana wakati wa bomoabomoa hiyo ni Shirika la Umeme (Tanesco) kuchelewa kukata umeme kwenye nyumba zinazotakiwa kubomolewa.
Alisema walilazimika kutumia zaidi ya dakika 20 kwa kila nyumba iliyokuwa na umeme ili kusubiri mafundi kufanya kazi hiyo.
“Wenzetu wa Tanesco wamekuja tukashirikiana nao, lakini hii ni changamoto kwa sababu imechelewesha kazi yetu kukamilika kwa wakati,” alisema.
NYUMBA ZENYE HATI
Kisigira alisema, takribani nyumba 10 ndiyo zilikuwa na hati miliki ya ardhi na hivyo hazikubomolewa.
Alisema hati hizo zilichunguzwa na wataalam kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ili kubaini uhalali wake.
“Kati nyumba hizi tulizobomoa ni takribani nyumba 10 tu zimebainika kuwa na hati miliki hivyo hatujazibomoa tunasubiri utaratibu wa tathmini ufanyike kwanza,” alisema.
HALI ILIVYOKUWA
Bomoabomoa ya nyumba hizo zilizoko Bonde la Msimbazi ilianza jana majira ya saa 4:30 asubuhi, huku likitumia Tingatinga tano na kuacha taharuki kwa wakazi wa maeneo hayo.
Akizungumza na Nipashe, mmoja wa wakazi wa eneo la Hananasif, Maria Wapalila, alisema bomoaboma hiyo imewatia hasara kutokana na kuingia gharama zisizo za lazima kutokana na kukodi watu wa kubomoa nyumba zao.
“Nyumba hizi tunatoa hela kwa  mafundi wanatubomolea kwa Sh. 100,000 hadi 200,000 kwa paa, dirisha na mlango tu, suala la kuhamisha ni watu wengine ambao nao wanatoza hadi Sh. 50,000,” alisema Wapalila.
Pia alisema ubomoaji huo umesababisha wao kupoteza mali zao kutokana na vibaka kuiba baadhi ya vyombo wakati wa kuhama.
 Naye, Sophia Shabani,  alisema kukodi vijana wa mitaani ambao siyo mafundi, wanatoza Sh. 30, 000 hadi Sh. 50,000 na wakimaliza kubomoa unatakiwa ulinde mali zako ili kuepuka wezi.
 “Eneo hili nilinunua tangu mwaka 2005 lakini lilikuwa halijai maji ila kwa miaka hii ya karibuni maji yameanza kufika hadi ndani kutokana na watu wengi kuendelea kujenga sehemu zenye vyanzo vya maji na miferejini,”alisema. 
Alisema ubomoaji wa nyumba zao ulianza tangu serikali ilipotoa siku 14 za kuwataka kubomoa kwa hiari ili kuokoa mali zao.
Halikadhalika katika maeneo hayo vijana mbalimbali walionekana wakiendelea na shughuli za kubomoa nyumba  zinazotakiwa kubomolewa kwa kuondoa mabati, milango na madirisha.
Wengine pia walionekana wakipita nyuma ya Tingatinga kuokota masalia ya nondo zilizokuwa zimejengea nyumba hizo.
MAHAKAMA YAPIGA ‘STOP’
Mahakama  Kuu Kitengo cha Ardhi, imesitisha mchakato wa ubomoaji wa  nyumba 674 kwa wakazi wa Kinondoni jijini Dar es Salaam hadi hapo shauri la msingi litakaposikilizwa na kutolewa uamuzi.
Uamuzi wa shauri hilo umekuja ikiwa siku moja baada ya  Mbunge wa Kinondoni, Maulid Mtulia (CUF)  na walalamikaji wanane kufungua kesi ya kupinga ubomoaji wa nyumba hizo.
Mbali na Mtulia wengine walioshiriki kufungua kesi hiyo na kuwawakilisha wenzao 674 ni Ally Kondo, Agnes Machalila, Sanura Abeid, Sultan Ally, Mussa Hassan, Gordwin Cuthbert na Rene Duma.
Kesi hiyo ambayo ilifunguliwa  juzi, yenye namba 822,  chini ya Jaji Penterine Kente, ilianza kusikilizwa lakini ilishindikana kutolewa uamuzi kutokana na mvutano mkali wa kisheria baina ya pande mbili. Hali hiyo ilisababisha kuahirishwa hadi jana.
Kabla ya kutolewa kwa uamuzi huo, saa nane alasiri, Jaji Kente alisema suala hilo limekuwa gumu kwake na kwamba katika mazingira ya haki, utawala bora na wa sheria licha ya kasoro ndogo ndogo zilizojitokeza haiondoi uzito wa uamuzi wa shauri hilo.
Alisema hoja kubwa ambayo inasubiriwa ni ombi la kuzuia ubomoaji wa nyumba 674 ambalo limewasilishwa na watu wanane, huku swali likiwa mahakama itaweza kutoa zuio la ubomoaji au la.
Hata hivyo, alisema hatua ya ubomoaji ni kwamba serikali ina nia njema na taratibu zote za kisheria zinafuatwa na mchakato huo umekuwa na athari kwa wanaobomolewa. 
 Alisema kutokana na hali ilivyo, mahakama imesitisha kubomolewa kwa nyumba za waombaji hao hadi hapo shauri la msingi lililofunguliwa kupinga ubomolewaji litakaposikilizwa na kutolewa uamuzi.
Aidha Jaji Kente alisema serikali inaweza kuendelea na mchakato wake wa kuweka alama na kuvunja nyumba ambazo hazitambuliki mahakamani na si kwa wale  waliowasilisha maombi yao.
 Baada ya kusema hayo, Jaji Kente alisema kuwa licha ya kutolewa kwa zuio hilo lakini kuna kesi ya msingi ambayo itaendelea kusikilizwa Januri 11, mwaka huu.
 Akizungumza nje ya mahakama hiyo, Mwanasheria wa  NEMC, Manchele Suguta, alisema pamoja na kuwekwa kwa angalizo hilo wataendelea na ubomoaji katika maeneo mengine kwa kufuata sheria hadi hapo uamuzi utakapotolewa dhidi ya kesi hiyo.
Hali ilivyokuwa mahakamani
Nje ya mahakama hiyo, jeshi la polisi liliimarisha ulinzi  tofauti na siku zingine kwani kulikuwa na gari la maji ya kuwasha na askari wa kikosi cha kuzuia ghasia walikuwa wakizunguka katika eneo hilo kutokana na umati wa wananchi waliohudhuria kufuatilia shauri hilo.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!