Friday 9 October 2015

KINGUNGE KUIPASUA CCM



Kada mkongwe wa zamani wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kingunge Ngombale Mwiru ameanza rasmi kazi ya kupanda jukwaani kukizamisha chama chake cha zamani baada ya kuwaambia wananchi wa Arusha kuwa wamchague mgombea urais wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa ili aingie Ikulu baada ya uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 25.

Kingunge aliyeitumikia CCM kwa miaka zaidi ya 60 kabla ya kukihama wiki iliyopita kwa madai kadhaa yakiwamo ya kupuuzwa misingi ya kuanzishwa kwake, aliwaambia maelfu ya wananchi waliojitokeza kwenye viwanja vya Sinon, Unga Limited mjini hapa kuwa Lowassa ndiye mgombea mwenye sifa zote za uongozi na hivyo, wanapaswa kuungana na Watanzania wengine katika kumpigia kura nyingi za ndiyo ili kuing’oa CCM madarakani.
Alisema kwa kufanya hivyo, ndipo Watanzania watakuwa na fursa ya kutoa nafasi ya kufanyika kwa mabadiliko ya kweli ya uongozi kwa manufa ya taifa. 
Kadhalika, aliwataka wananchi kuchagua pia wagombea wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) vya Chadema, Chama cha Wananchi (CUF), NCCR-Mageuzi na NLD ili kuiondoa kabisa CCM katika kila ngazi. Mbali na kupeperusha bendera ya Chadema, Lowassa pia anawakilisha Ukawa.  
“Mnapofika kwenye vituo vya kupigia kura, mchagueni Lowassa... na pia wabunge na madiwani wa Ukawa,” alisema na kuibua shangwe kubwa kutoka kwa watu waliojitokeza kwenye mkutano huo.
Akieleza zaidi, Kingunge alirudia kauli yake aliyoitoa wiki iliyopita wakati akitangaza kujiondoa CCM kwa kusema kuwa chama chake hicho cha zamani kimeshaishiwa pumzi na hivyo hakina tena uwezo wa kuiongoza Tanzania, ushahidi ukiwa ni kushindwa kwake kuinua uchumi.
“CCM pumzi imekwisha. Wale wenye pumzi ndiyo watakaoweza kufika kileleni... tunahitaji mabadiliko ili tuweze kupambana na umasikini na kuinua uchumi kwa asilimia 10,” alisema na kuongeza:
“Mimi ni mtu wa mabadiliko. Nina historia yangu... nimeshiriki katika kuleta mabadiliko na nimeamini kutoka ndani ya moyo wangu kuwa mabadiliko Tanzania ni lazima,” alisema.
Aidha, alisema amekuwa akifuatilia kampeni za vyama vya siasa lakini ameshangazwa na kilichokuwa chama chake kuamua kupiga kampeni za ‘majitaka’, kwa kuruhusu watu kuwashambulia wengine wenye mitazamo tofauti badala ya kueleza sera na kutoa ahadi kwa wananchi wanaotaka wawachague.
“Nimekuwa nikifuatilia kampeni zinazoendelea nchini. Ukawa wametia fora... wameonyesha ustaarabu, utulivu na heshima kwa nchi yetu,” alisema.
“Kwa bahati mbaya, CCM ambayo ilikuwa ni chama changu, tangu walipoanza kampeni wanafanya maajabu na vituko. Walianza kampeni za matusi ya kustaajabisha. Licha ya CCM kuwa na sera nyingi, lakini hawazungumzii sera. Wanazungumzia mtu,” alisema.
Aliongeza kuwa kuna watu wazima na wengine wamestaafu, lakini wote wamechukuliwa na kupandishwa majukwaani kwa sababu moja tu ya kumzungumzia mtu mmoja.
“Ukiona kila mtu anamzungumzia mtu mmoja, tena huyo huyo... jua kuwa mtu huyo atakuwa ni mzito sana. Siasa si uadui,” alisema.
Kuhusu marafiki zake waliobaki CCM, Kingunge alisema anawataka kutobabaika na badala yake wamchague rais wanayemtaka.
“Nimewaacha CCM kwa sababu siwezi kukubaliana na uongozi unaovunja katiba za chama, taratibu za chama na unaowadhalilisha wagombea wa urais. Kila mtu ana haki ya kumchagua rais anayemtaka,” alisema.
LOWASSA ATAKA KURA NYINGI
Wakati akizungumza jana, Lowassa alirudia tena kauli yake ya kuwataka wananchi wajitokeze mapema siku ya kupiga kura na kumpa kura nyingi za ndiyo ili kukabiliana vyema na vitendo vya wizi wa kura vinavyoweza kufanywa na CCM.
Alisema jambo hilo ni muhimu kwani CCM ina historia ndefu ya wizi wa kura na hivyo, njia pekee ya kuikabili hali hiyo ni kupiga kura nyingi zaidi ili hata wakiiba, athari zake zisimnyime ushindi.
“Naomba kura nyingi kwa sababu hawa jamaa wana historia ya wizi wa kura. Pigeni kura nyingi,” alisema. 
Akizungumzia uamuzi wa Kingunge, Lowassa alisema kuondoka CCM kwa kada huyo mkongwe ni pigo kubwa na pia ni ishara nzuri ya kuwadia kwa mabadiliko.
“Kingunge ni mzee lakini anaonekana kama kijana wa miaka 20...  hili ni pigo kwa CCM,” alisema.
HUDUMA ZA AFYA
Akizungumzia huduma ya afya, Lowassa alisema iwapo atachaguliwa kuwa rais atahakikisha kunakuwa na hospitali za wilaya katika kila wilaya nchini.
Kadhalika, alisema akiingia madarakani, ataunda serikali makini itakayoshughulikia matatizo ya Watanzania.
Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye, alisema tangu CCM iingie madarakani hali ya uchumi imezidi kudidimia kutokana na ubadhilifu unaofanywa na viongozi wa chama hicho na hivyo ni wakati mzuri sasa kwa Watanzania kufanya mabadiliko kwa kumchagua Lowassa na wagombea wote wa Ukawa.
Mwenyekiti wa NCCR - Mageuzi, James Mbatia, aliituhumu CCM kwa kubebwa na serikali kupitia vitendo mbalimbali vyenye kuiwezesha kupata fedha kwa njia haramu ili kuinufaisha.
HALI ILIVYOKUWA ARUSHA
Kabla ya kufanyika kwa mkutano huo jijini Arusha jana, maelfu ya watu walijitokeza mapema asubuhi, kuanzia saa 5:00 asubuhi huku magari na pikipiki zikipita huku na huko, zikipambwa kwa bendera za Chadema. 
Baadhi ya maduka yalifungwa na shughuli mbalimbali zilisimama.
Hata hivyo, amani ilitawala muda wote huku magari ya Jeshi la Polisi yakiranda randa huku na huko kulinda usalama.
Hadi kufikia saa 8:00 mchana, uwanja huo wa Sinon tayari ulikuwa umefurika hadi watu wengine kuonekana wakikosa sehemu nzuri za kukaa.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!