Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) imewataka wananchi kujitokeza kuhakiki taarifa zao kwenye daftari la wapiga kura kwa kuwa mwisho wa zoezi hilo ni keshokutwa.
Taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi Mkuu wa Nec, Kailima Kombwey, kwa vyombo vya habari jana, ilisema zoezi hilo lilianza Agosti 19 mwaka huu na linatarajiwa kumalizika Septemba 7. Daftari la awali la Wapiga Kura limewekwa wazi katika kata zote za jiji la Dar es Salaam.
Mashine za Biometric Voter Registration (BVR) zinazotumika kufanyia marekebisho zimewekwa katika kata zote ili wananchi wapate huduma hiyo.
Taarifa hiyo ilieleza madhumuni ya zoezi hilo ni kurekebisha taarifa za Mpiga Kura zilizokosewa wakati wa uandikishaji, kutoa kadi mpya kwa wapiga kura waliopoteza kadi zao na wamo katika Daftari la awali la Wapiga Kura.
Kuondoa wapiga Kura waliofariki au waliokosa sifa kwa mujibu wa sheria, Kuhamisha taarifa za wale waliohama toka kata au Jimbo kwenda Kata au Jimbo lingine, kutoa nafasi kwa wapiga kura walioandikishwa kukagua taarifa kama zipo kwenye daftari.
Alisema wenye kadi za mpiga kura lakini majina yao hayaonekani katika daftari la awali la wapiga kura watafanyiwa uhakiki katika mifumo ya BVR na iwapo itathibitika kuwa wamo watarudishwa katika mfumo wa daftari.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo mtu anaweza kukagua taarifa zake kwa njia ya simu kwa kubonyeza *152*00# au tovuti www.nec.go.tz na kufuata maelekezo.
No comments:
Post a Comment