
NA MWANDISHI WETU, DODOMA
HATIMAYE Sheikh Abubakar Zubeir amechaguliwa kuwa Mufti Mkuu wa Tanzania, katika Mkutano mkuu wa Baraza Kuu la Wasilamu Tanzania (BAKWATA), uliofanyika mkoani hapa.
Sheikh Zubeir amechaguliwa kushika wadhifa huo, baada ya kifo cha aliyekuwa Mufti wa Tanzania, marehemu Sheikh Issa Shaaban Simba, aliyefariki Juni, 2015.
Akizungumza katika mkutano huo wa kumpata Mufti, uliohusisha wajumbe takribani 310, Sheikh wa Mkoa wa Dodoma, Salum Mussa, aliyekuwa Mwenyekiti, alisema Sheikh Zubeir amechaguliwa kushika wadhifa huo baada ya kukosa mpinzani.
Kabla ya kuchaguliwa rasmi Sheikh Zubeir alikuwa akikaimu nafasi hiyo.
Alisema Shekhe Zubeir alikuwa na wapinzani watatu katika kuwania wadhifa huo ambao ni Sheikh Ally Mkoyogole, Sheikh Hassan Kiburwa na Sheikh Khamis Mtupa.
“Wagombea wawili walienguliwa katika kikao cha Baraza za Ulamaa ambao ni Mtupa na Kiburwa kutokana na kukosa vigezo,” alisema.
Wagombea wawili walibaki Sheikh Mkoyogole na Sheikh Zubeir walikwenda kujadiliwa na Tume ya Dini inoyohusisha masheikh wote wa mikoa na wilaya na ndipo Sheikh Mkoyogole alitangaza kujitoa.
“Tutashirikiana na kuijenga BAKWATA katika masuala ya maendeleo na kukabiliana na changamoto mbalimbali kwa kujenga umoja na ushirikiano,” alisema Sheikh Zubeir baada ya kuchaguliwa.













No comments:
Post a Comment