Monday 20 October 2014

FAHAMU UMUHIMU WA KULA DAGAA KWA AFYA YAKO

Kwa imani ya watu wengi, dagaa ni kitoweo cha kimaskini, huonekana kuwa kununua dagaa sokoni au ‘super market’ kwa ajili ya kitoweo, ni dalili ya muhusika kuishiwa au kuwa na bajeti ndogo.



Tunapoangalia umuhimu wa dagaa na faida zake katika mwili wa binadamu, tunagundua kuwa uwe maskini, tajiri au bilionea, kama unajali afya yako, dagaa ni muhimu kula kuliko mapochopocho unayokula kifahari.
Katika makala hii tutaangalia faida za kiafya za dagaa, wana faida kubwa sana katika kupambana na kutoa kinga ya magonjwa hatari ya moyo!
FAIDA KWA AFYA YA MOYO
Kama ilivyo kawaida, dagaa nao wameonesha kuwa na faida kubwa kwa wenye matatizo ya magonjwa ya moyo. Dagaa wana virutubisho vingi na miongoni mwa virutubisho hivyo kuna kiwango kikikubwa cha Omega-3 Fatty Acids (EPA & DHA).
Katika tafiti nyingi za magonjwa ya moyo na tiba zake, virutubisho vya Omega 3 vimeonekana kuwa dawa au kinga kubwa sana ya magonjwa ya moyo. Chanzo kikuu cha virutubisho hivyo si vingine bali ni samaki pamoja na dagaa.

Aidha, dagaa pia ni chanzo kizuri cha Vitamin B12, ikiwa ni chanzo kizuri cha pili baada ya maini. Vitamin hii hufanyakazi kubwa ya kuboresha ustawi wa moyo na hivyo kuwa chakula kizuri cha kumpa ahueni au kinga madhubuti mlaji dhidi ya magonjwa ya moyo.

AFYA YA MIFUPA
Dagaa ni chanzo kingine kizuri cha madini ya ‘Calcium’ yenye jukumu la kuimarisha mifupa ya mwili, lakini pia kwenye dagaa kuna vitamin D ambayo huwa nadra sana kupatikana kwenye lishe.

Vitamin D hufanyakazi muhimu ya kuimarisha afya ya mifupa kwani ndiyo inayosaidia unyonywaji mwilini wa madini ya ‘calcium’. Vile vile dagaa ni chanzo kizuri cha madini aina ya ‘phosphorus’, ambayo nayo huimarisha mifupa.

DAGAA NA KANSA
Kwa miaka mingi, watafiti wameona jinsi ambavyo dagaa inavyoweza kudhibiti seli zinazosambaza saratani mwilini. Hivyo imethibitika pasipo na shaka kuwa virutubisho vilivyomo kwenye dagaa huweza kutoa kinga kubwa dhidi ya ugonjwa wa saratani.

WAMEJAA PROTINI
Kama una upungufu wa protini mwilini, basi kula dagaa kwani wao wana kiwango kikubwa cha kirutubisho hicho. Protini husaidia uzalishaji wa ‘Amino acids’ ambazo ni muhimu kwa uzalishaji wa chembe hai mwilini na uimarishaji wa mfumo wa kinga ya mwili (body immune system).

TAHADHARI
Wagonjwa wa figo na wale wenye matatizo ya ‘gout’, wanashauriwa kula dagaa kiasi kidogo na kwa tahadhari kubwa au kuepuka kabisa. Sababu inayotolewa ni kwamba, kama ilivyo kwa baadhi ya vyakula vingine, dagaa huwa na vitu (purine) ambavyo vinaweza kuwasumbua watu wenye magonjwa hayo, vinginevyo dagaa siyo chakula cha kukosa kula!

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!