.jpg)
Kamanda wa Polisi katika Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, ametoa muda wa wiki moja kwa makamanda wa Polisi wa mikoa ya kanda hiyo, kushirikiana na wananchi, ili kuwasaka na kuwatia mbaroni vijana wanaojiita ‘mbwa mwitu’ wanaotishia usalama wa watu jijini.
Vijana hao wamekuwa wakifanya uhalifu katika maeneo mbalimbali ya Jiji na kusababisha hofu miongoni mwa wananchi.
Pamoja na kupora mali za watu, mbwa mwitu pia wamekuwa wakiwajeruhi wananchi kwa mapanga na silaha nyingine za kijadi.
Mwishoni mwa Desemba mwaka jana, vijana hao walifanya uhalifu mkubwa katika maeneo ya Kiwalani na Yombo kwa Limboa na baadaye Tabata Kisiwani na Mabibo.
Hata hivyo polisi walikwenda katika maeneo hayo na kuendesha msako mkali uliowezesha kukamatwa kwa baadhi ya vijana na wengine walikimbilia mikoani.
Lakini makundi ya vijana hao, yanazidi kuenea katika mitaa mingine mithili ya moto wa vifuu na kutishia maisha ya watu.
Kamanda Kova alikiri kuwapo kwa tatizo hilo na kwamba wamekubaliana kila mkoa wa kipolisi, uwasake na kuwatia mbaroni vijana hao.
Kwa mujibu wa kamanda huyo, msako wa awali uliwezesha kukamatwa kwa “mbwa mwitu 169 ambao alisema wanaendelea kuhojiwa na polisi.
“Kwa hiyo sasa nimetoa wiki moja kwa makamanda wangu wawe wameshawakamata vijana hao wanaojiita mbwa mwitu ili kuwawezesha wananchi kuishi kwa amani,”alisema Kova
Alielezea matumaini yake kuwa kama wananchi watashirikiana na polisi, mtandao wa vijana hao unaweza kuangamizwa













No comments:
Post a Comment