Thursday 10 October 2013

MFANYABIASHARA MWINGINE MAARUFU AMWAGIWA TINDIKALI,ARUSHA....




Hospitali ya Seliani ambako mfanyabiashara huyo amelazwa kwa matibabu


Mfanyabiashara Japhet Minja amelazwa katika Hospitali ya Arusha Lutheran Centre (Seliani) jijini Arusha, baada ya kumwagiwa kimiminika kinachosadikiwa kuwa tindikali usoni na watu wasiojulikana.

Minja alitendewa unyama huo jana saa 12.15 alfajiri eneo la Shamsi wakati akitoka nyumbani kwake kwenda kazini.
Akisimulia tukio hilo, mmoja wa ndugu wa Minja ambaye hakutaka kutaja jina lake, alidai Minja alikutwa na mkasa huo wakati akiendesha gari lake kwenda katika shughuli zake za kawaida.
Alidai baada ya kufika eneo la Shamsi alikutana na vijana wanne wakiwa wamesimama barabarani, wakamsimamisha kama vile watu waliokuwa wakiomba msaada.
“Baada ya ndugu yangu kusimama, alishusha kioo cha gari upande wake na hapo wale vijana wakafungua mlango kwa nguvu na kumchomoa ndani ya gari na kumtoa nje.
“Baada ya hapo walimshambulia kwa kumpiga na kummwagia tindikali usoni,” alidai.
Alidai baada ya kumwagiwa tindikali, watu waliokuwa karibu na eneo hilo walijaa na vijana hao walikimbia na kutokomea kusikojulikana.
Hata hivyo waandishi waliotembelea Hospitali ya Seliani kuonana na mgonjwa, hawakuruhusiwa kwa madai kuwa mgonjwa huyo yupo chumba cha uangalizi maalum (ICU).
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas, akizungumzia tukio hilo alisema kuwa Polisi wanaendelea na uchunguzi.
“Kitu kinachotupa mashaka ni kimoja… yule mtu aliendesha gari mwenyewe, sasa kama ni tindikali utaweza kuendesha gari kweli, hivyo vitakuwa visa tu,” alidai Kamanda Sabas.
Sabas alidai kuwa hata uso wake haujaathirika kama watu wanavyosema, japo ameumia kidole ambacho anadai aling’atwa na watu hao waliomvamia.
Alisema kijana huyo anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 30 ni mfanyabiashara na anatengeneza madirisha ya aluminium.

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!