Thursday 25 January 2018

Mwanafunzi abakwa na kuuawa akienda shule

MWANAFUNZI wa kike mwenye umri wa miaka 14 ameuawa kikatili baada ya kubakwa kwa zamu na mwendesha pikipiki maarufu ‘bodaboda’ kisha akachomwa kisu ubavuni na sehemu zake za siri kunyofolewa wakati akienda shule akiwa amefuatana na mdogo wake wa kiume mwenye umri wa miaka 11.


Mwanafunzi huyo alikuwa akisoma darasa la sita katika Shule ya Msingi Vikonge katika wilaya ya Tanganyika mkoani Katavi, sambamba na mdogo wake wa kiume ambaye alikuwa akisoma darasa la nne kwenye shule hiyo. Kamanda wa Polisi mkoa wa Katavi, Damas Nyanda alisema kuwa tukio hilo la kikatili lilitokea juzi Jumanne saa moja asubuhi umbali wa kilometa moja na nusu kutoka shuleni hapo.
“Asubuhi hiyo ya tukio, marehemu akiwa ameongozana na mdogo wake wa kiume huku wakielekea shuleni walikutana na mwendesha pikipiki maarufu ‘bodaboda’ ambaye alikuwa hawamfahamu na kuwaambia kwamba atawapa lifti. Marehemu alipopanda mwendesha bodaboda alimzuia mdogo wake wa kiume asipande ambapo aliondoka akiendesha pikipiki hiyo kwa kasi isiyo ya kawaida huku kaka wa marehemu akiikimbilia bila mafaniko.
Aliongeza kuwa mdogo wa marehemu alipoamua kutembea kwa miguu kuelekea shuleni baada ya kuchoka kuifukuza pikipiki hiyo, ghafla aliiona pikipiki ile iliyombeba dada yake ikiwa imeegeshwa karibu na kichaka kando ya barabara inayoelekea shuleni kwao na akaipita.
Kamanda Nyanda alisema kaka huyo wa marehemu alienda shuleni hapo na kuhudhuria darasani kama kawaida hadi ilipofika saa nane na nusu alianza safari kuelekea nyumba pasipo kumtafuta dada yake.
“Kaka wa marehemu bila shaka kutokana na umri wake kuwa bado mdogo baada ya kufika shuleni hakushughulika kumtafuta dada yake, aliingia darasani na kuendelea na masomo kama kawaida na baada ya muda wa masomo yaani saa nane na nusu alianza safari ya kurejea nyumbani bila kumtafuta dada yake,” alieleza Kamanda Nyanda.
Aliongeza kuwa baada ya mtoto huyo kufika nyumbani wazazi wake walishtuka kumuona akiwa pekee yake ndipo walipomuhoji alikomuacha dada yake ndipo alipowasimulia kila kitu.
“Wazazi wa marehemu baada ya kupata maelezo hayo walipatwa na mashaka hivyo walimtaka mdogo wa marehemu awapeleke kwenye eneo alipoina pikipiki iliyombeba dada yake ikiwa imepakiwa karibu na kichaka. Mtoto huyo aliwaongoza wazazi wake ambao walikuwa wamefutana na majirani zao hadi kwenye eneo la tukio, walishtuka kuona kuwa kuna nyasi zilikuwa zimelala ndipo walipoona mwili wa marehemu ukiwa umechomwa kisu ubavuni huku sehemu zake za siri zikiwa zimenyofolewa.

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!