Saturday 18 March 2017

Filamu ya Kiumeni iwafungue macho waigizaji nchini





JUMATANO ya wiki hii, tasnia ya filamu ilipata mwanga mpya kufuatia filamu ya Kiumeni kuanza kuoneshwa rasmi kwenye kumbi za filamu nchini.


Filamu hiyo sio ya kwanza kuanza kuoneshwa kwenye kumbi za Sinema ila ni filamu ambayo ninaweza kusema kuwa ni kati ya filamu chache zenye viwango kuwahi kutengenezwa hapa nchini.
Huku ikiwa imetengenezewa kwenye mazingira ya kawaida kabisa ya kitanzania na tena asilimia 90 ikiwa imtetengenezwa eneo la Kigogo, Dar es Salaam.
Kikubwa ambacho wasanii wa tasnia ya filamu hapa nchini wanatakiwa kujifunza ni namna ambavyo mpangilio wa filamu hii ulivyo na unavyovutia.
Imekuwa kwa muda mefu filamu za kitanzania zimekuwa zinaboa na zimekuwa hazina mvuto hali inayopelekea kushuka kwa soko la filamu nchini.
Filamu za kibongo zimekuwa zikionekana ni zina stori zilezile na huku zaidi zikiwa zinagusia mapenzi au ahata kiwango chake cha uigizaji, utengenezwaji au hata upigwaji wake wa picha ukiwa ni uleule.
Katika filamu ya Kiumeni licha ya kuwa imeigiziwa mazingira ya kawaida kabisa lakini wahusika wameweza kuteka nyoyo za wapenzi wa filamu kutokana na mpangilio wa matukio.
Matukio hayo yanachekesha na yanavutia huku wahusika wakiwa wanajua kuuvaa uhalisia wa kila kipengele wanachoshiriki.
Kikubwa katika uigizaji wa filamu ni namna ambavyo waigizaji wanaweza kufuata mwongozo wa uigizwaji au hata pia mwongozo wenyewe umeandikwaji na unaongozwaje.
Lakini pia hata namna ya kamera zilivyokuwa zikitegeshwa na kutumika katika namna ya upigwaji wa picha pamoja na kuonesha lengo husika lililokusudiwa.
Binafsi ninapendekeza kuwapo kwa mjadala wa mara kwa mara kati ya waigizaji wa filamu wa kitanzania kukaa kujadiliana kuhusiana na filamu na kujinoa kielimu ili kuboresha zaidi.
Kama watengenezaji wa filamu wakiwa na hulka ya kutengeneza filamu zenye kiwango na kuzingatia weledi katika sekta hiyo ya filamu soko lipo, kwa kuwa watazioesha kwenye kumbi za sinema na watanzania wataenda kuziona.
Kama ilivyokuwa kwa mhusika mkuu wa filamu ya Kiumeni ambae pia aliigiza filamu ya Going Bongo, Ernest Napoleon alivyoweza kuuvaa uhusika huku mwongozaji wa filamu hiyo Nicolas Marwa akiiongoza kiufundi.
Ikumbukwe kuwa filamu za kiswahili zinaweza kuwa na soko kubwa katika nchi za Afrika Mashariki na Kati kwa kuwa wengi wanazungumza lugha hiyo, hivyo soko linaweza kuwa kubwa kama waigiaji wakitengeneza kwa lengo la kuzionesha kwenye kumbi za filamu, Cinema halls.
Kama alivyofanya Ernest kuanzia kwenye filamu ya Going Bongo ambayo hadi sasa inaoneshwa kwenye nchi mbalimbali kama vile Zimbabwe, Kenya Afrika Kusini ambapo Kiumeni licha ya kuwa ni ya kiswahili na inaweza kuoneshwa kwenye nchi zinazotumia lugha hiyo lakini pia hata zile zinazotumia lugha ya Kiingereza sababu ina maandishi ya lugha hiyo.(Subtitles).
Waigizaji na waongozaji wa filamu za kitanzania hawana budi kwenda Mlimani kujifunza kitu kutokea kwenye filamu ya Kiumeni ili iwe changamoto kwao kuigiza filamu zenye kiwango kama hicho ambacho hata gharama yake sio kubwa.

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!