Saturday 2 July 2016

UCHUNGUZI UNAENDELEA KUBAINI BAWA LA NDEGE LILILOOKOTWA NA WAVUVI KATIKA KISIWA CHA KOJANI PEMBA

PEMBA-ZANZIBAR
MAMLAKA ya Usafiri wa Anga Tanzania  imesema uchunguzi  wa kitaalamu bado unaendelea ili  kubaini iwapo bawa la ndege lililookotwa na wavuvi  katika Kisiwa cha Kojani Pemba ni  mabaki ya ndege  ya Malyasia . 

Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka hiyo Vallery Luanda Chamlungu ameyabainisha hayo wakati wa makabidhiano ya  bawa hilo yaliyofanyika  katika bandari ya Kojani na kushuhudiwa na Viongozi wa mbali mbali wa Serikali wakiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Wete .
Alisema , pamoja na uchunguzi wa kitaalamu unaofanywa na mamlaka hiyo , lakini pia Uongozi unaendelea kuwasiliana na mashirika ya ndege ya  kimataifa ya ili kusaidia kukamilisha machakato wa kutambua asili ya ndege hiyo .
“Uchunguzi bado unaendelea ili kubaini kwamba bawa hilo ni mabaki ya ndege ya Malyasia iliyopotea miaka kadhaa iliyopita , tunafanya mawasiliano na mashirika ya ndege ya kimataifa na hili bawa tunatarajia wenzetu kutoka  Malyasia watakuja  ”alifahamisha Chamlungu .
Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka hiyo alisema wataendelea kushirikiana na wananchi kufanya utafiti hasa sehemu za baharini sambamba na kuwashukuru wavuvi wa Kojani kwa kuweza kulihifadhi bawa hilo .
Aidha , Mkuu wa Wilaya ya Wete Rashid Hadid Rashid akikabidhi bawa hilo   aliwataka wananchi kuwasiliana na vyombo vya ulinzi wanapookota vitu  baharini , na kuacha kuvihifadhi majumbani kwani baadhi vinaweza kuwa ni hatari kwa maisha yao .
Alisema , Serikali ya Wilaya ilisimamia ili kuona kwamba bawa hilo linahifadhiwa , na linabaki  katika mazingira yaliyo salama ili kupisha uchunguzi wa kitaalam ufanyike .
“Pamoja na juhudi zenu , lakini pia naomba nitoe wito kwa wavuvi kutoa taarifa Serikalini ili kuepisha utokea kwa madhara yasiyotarajiwa  , baada ya kuhifadhi majumbani mwenu ” alisisitiza Mkuu wa Wilaya.
Mmoja wa mashuhuda waliookota bawa hilo Chungua Hamad Chungua aliishauri mamlaka ya Usafiri wa Anga kuwaandalia mazingira mazuri ya kuwapatia mashine ya uvuvi ambayo itawasaidia  katika kazi zao za uvuvi .
Alisema ,  ni vyema Mamlaka hiyo kuwazawadia mashine ya supa kumi au kumi na tano kutokana na usumbufu walioupata wakati wa kulikokota kwani ni zito na bahari ilikuw aimechafuka .
Hata hivyo Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga iimekabidhi shilingi milioni mbili wavuvi waliofanikisha kuliokota na kulihifadhi kama ni zawadi .
Kwa mujibu wa taratibu na sheria , Mamlaka ya Usafiri wa Anga haina ulazima wa kuwalipa wananchi wanaokota vitu aidha baharini au nchi kavu , isipokuwa hulazimika kutoka zawadi ili kuwajenga imani wananchi ya kuvihifadhi vitu wanavyo viokota

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!