Monday 11 April 2016

TUMEKUWA KIMBILIO KWA MAGONJWA MAKUBWA

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema Tanzania imeanza kuwa kimbilio katika utoaji wa huduma za matibabu ya moyo na figo, kwa wagonjwa kutoka nchi za jirani.


Alisema hayo jana alipotembelea hospitali ya Benjamini Mkapa, iliyopo katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM).
Majaliwa alisema, Serikali itaimarisha huduma hizo katika hospitali hiyo, Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) na Hospitali ya Mloganzila, ziwe vituo vya kitaaluma ili wananchi wapate manufaa ya uwepo wake.
Alisema, kupatikana kwa huduma hizo za magonjwa makubwa nchini kutasaidia kuondoa gharama ambazo Serikali huingia kuwapeleka Watanzania kutibiwa nje ya nchi.
“Hivi sasa Taasisi ya Jakaya Kikwete imeanza kutibu magonjwa ya moyo na upasuaji. Tunataka matibabu yote ya figo, hata ya kubadilisha figo yafanyike ndani ya nchi, hilo linawezekana. Wataalamu tunao, tena wengi ni Watanzania na wanafanya kazi nyumbani kwa moyo wakijua kuwa wanaokoa maisha ya ndugu zao na wazazi wao,” alisema Waziri Mkuu.
Alisema, uwepo wa hospitali hizo ni kimbilio kwa Watanzania na kwa wagonjwa wanaotoka nchi jirani, ambapo kwa sasa Tanzania imeanza kupokea wanaotoka Malawi, Msumbiji, Comoro, Kenya na Uganda. Alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ulinzi katika kituo hicho, ili vifaa vilivyopo viendelee kuwepo.
Aliongeza kuwa, Serikali imeamua kuiwezesha hospitali ya Benjamini Mkapa ijitosheleze kwa kutoa huduma za matibabu kwa wakazi wa Kanda ya Kati, Kanda ya Ziwa na Kanda ya Magharibi, ili kuwapunguzia gharama za kwenda Muhimbili.
“Hivi sasa kuna vyuo vikuu hapa nchini vinavyosomesha Watanzania utaalamu wa juu wa tiba, ikiwemo UDOM, chuo hiki kitakuwa kituo cha Watanzania kupata taaluma ya tiba kwa magonjwa yote makubwa, ili wananchi wapate manufaa ya uwepo wake,” alisema.
Pamoja na hayo, alisema kuna changamoto ya baadhi ya mashine kukaa nje ya vyumba vilivyokusudiwa na kushindwa kufungwa kutokana na udogo wa vyumba ikilinganishwa na ukubwa wa mashine.

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!