Sunday 27 March 2016

MAHAKAMA YATAKIWA KUEPUKA KUTOA HUKUMU KAMA PILATO

WATENDAJI wa Mahakama wametakiwa kuonesha tofauti ya hukumu zao na zenye utata kama iliyotolewa na Pilato kwa Yesu Kristo.


Paroko wa Kanisa Katoliki, Parokia ya Mtakatifu Bikira Maria Mpalizwa Mbinguni, Jimbo la Tunduru Masasi, Dominick Mkapa, alisema hayo juzi mjini hapa, wakati wa Ibada ya Ijumaa Kuu iliyofanyika katika kanisa hilo.
Kwa mujibu wa Paroko huyo, hukumu ya kifo iliyotolewa na Pilato wakati huo, ilijaa utata na uongo, mazingira yaliyosababisha Yesu Kristo, auawe kwa makosa ambayo hakutenda.
Alisema kushindwa kwa Pilato kusimama katika haki, woga pamoja na shinikizo kutoka kwa Wayahudi, ni baadhi ya sababu zilizofanya Yesu Kristo ahukumiwe, asulubiwe msalabani na hatimaye kifo na kuongeza kuwa sababu kama hizo hutumika hata sasa katika baadhi ya hukumu.
Paroko Mkapa alisema hata makosa aliyoshitakiwa Yesu, hayakuwa na ukweli wowote na alionesha wazi kusikitishwa na uamuzi wa Pilato wa kutoa hukumu kubwa kwa sababu ya shinikizo kutoka kwa Wayahudi.
“Nitoe mwito katika Ibada hii ya Ijumaa Kuu kwa mahakama nchini, zitoe adhabu katika misingi ya haki na usawa na bila shinikizo kutoka kwa mtu yeyote, ili kuepuka kutoa hukumu zenye utata na uonevu kama aliyopewa Bwana Yesu Kristo. “Hukumu iliyotolewa na Pilato wakati wa utawala wa Warumi chini ya Mfalme Kaiseri…haina tofauti na baadhi ya hukumu zinazotolewa hivi sasa katika baadhi ya mahakama nchini, hivyo ni vyema wanaokutwa na makosa wakatendewa haki,” alisema Mkapa.
Paroko Mkapa alisema mateso ya Yesu Kristo na kifo chake ni fundisho kwa Watanzania ambapo wanapaswa kuishi kwa amani na upendo kama inavyompendeza Mungu. Ibada hiyo pia ilihudhuriwa na Rais mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa ambaye yuko mjini Masasi kwa mapumziko ya Sikukuu ya Pasaka.

HABARI LEO

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!