Monday 14 December 2015

Dawasa yasaini bilioni 71/- za kujenga mtandao wa maji Dar Mkataba huo unamtaka mkandarasi kukamilisha kazi ndani ya miezi 15 kuanzia sasa na hivyo mradi huo... utaanza kuwanufaisha wananchi kuanzia mwaka 2017.




 Mamalaka ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (Dawasa), imesaini mkataba wa Dola milioni 32.97 za Marekani (sawa na Sh. bilioni 71) kwa ajili ya kujenga mtandao mpya wa mabomba ya maji kwa wakazi wa Dar es Salaam.
 
Mtandao huo utajenga mabomba kutoka Tegeta hadi Bagamoyo na Mbezi mpaka Kiluvya kwa lengo la kuwapatia maji wateja ambao hawajaunganishwa na mfumo rasmi. 
 
Mkurugenzi wa Huduma za Ufundi wa Dawasa, Romanus Mwang’ingo, aliyasema hayo jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki wakati akitoa maelezo ya miradi mbalimbali inayotekelezwa na mamlaka hiyo.
 
Mwang’ingo alisema mkataba huo uliosainiwa hivi karibuni na Serikali ya India na Benki ya Dunia (WB) umeiwezesha mamlaka hiyo kupata Dola milioni 32.97 za Marekani.
 
Alisema taratibu za kumpata mkandarasi zimekamilika na anatarajiwa kuanza kazi hiyo wakati wowote kuanzia sasa.
 
Mwang’ingo alifafanua kuwa mkataba huo unamtaka mkandarasi kukamilisha kazi ndani ya miezi 15 kuanzia sasa na hivyo mradi huo utaanza kuwanufaisha wananchi kuanzia mwaka 2017.
 
“Kwa wakazi wa Dar es Salaam na Pwani, wataanza kuona matunda ya mradi huu utakapokamilika na kuondokana na mgawo na shida ya maji inayowakabili wateja wa maeneo haya ,” alisema.
 
Aliongeza kuwa Dawasa inaendelea na utekelezaji wa miradi ya kuboresha huduma kwa wakazi waishio katika eneo lake la huduma ambalo ni Dar es Salaam, Kibaha na Bagamoyo.
 
Mwang’ingo alisema miradi hiyo inakwenda pamoja na upanuzi wa mitambo ya Ruvu Juu na Chini, uchimbaji wa visima vya maji baridi vya Mwambani eneo la Kimbiji, Mpera na ujenzi wa bwawa la Kidunda na mfumo wa ukusanyaji na kutibu majitaka.
 
Alifafanua kuwa lengo la miradi hiyo ni kuongezeka maji kutoka lita milioni 300 za sasa hadi milioni 756 mwakani.
 
Aliongeza kuwa kwa sasa mahitaji ya maji kwa wateja wa Dawasa ni lita milioni 450, hivyo baada ya kukamilika kwa miradi hiyo, maji yanatarajiwa kutosheleza wakazi hadi mwaka 2027.
 
Alisema mradi wa ulazaji wa bomba kutoka Ruvu Chini lenye kipenyo cha mita 1.8 hadi Chuo Kikuu cha Ardhi Dar es Salaam, unaelekea kukamilika baada ya kufanyika kwa asilimia 94.2.
 
 “Kazi hiyo ya ulazaji wa bomba kuu kutoka Ruvu Chini itakamilika Februari, mwakani na upanuzi wa miradi wa Ruvu Juu kutoka uzalishaji wa lita milioni 82 hadi lita 196 kwa siku, nao utakamilika mwezi ujao,” alisema.
 
Aliongeza kuwa ulazaji wa bomba kubwa eneo la Salasala unaendelea baada ya Dawasa kushinda kesi 13 kati ya 17 zilizokuwa mahakamani zilizofunguliwa na wananchi waliojenga katika hifadhi ya Dawasa.
 
Alisema kuwa baada ya kusafisha njia ya kupitisha mabomba hayo kwa kubomoa nyumba zilizojengwa kwa makosa, mkandarasi yupo eneo la mradi na anatarajiwa kukamilisha kazi hiyo mwakani.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!