Tuesday 9 June 2015

SERIKALI YAFUTA UMILIKI WA MASHAMBA YA WAWEKEAJI

Serikali imefuta umiliki wa baadhi ya mashamba yaliyokuwa yanamilikiwa na wawekezaji na kuyakabidhi kwa wananchi.

Kauli hiyo ilitolewa jana na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi wakati akiwasilisha hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa wizara yake katika kipindi cha 2015/2016.
Lukuvi alisema migogoro mingi kati ya wananchi na wamiliki wa mashamba, wananchi na hifadhi za Taifa imepungua baada ya mipaka kurekebishwa.
“Rais amefuta umiliki wa shamba la Ufyomi Galapo Estate na kazi inayoendelea kwa sasa ni kuhakiki, kupima na kumilikisha ardhi kwa wananchi ili waweze kuitumia,” alisema Lukuvi.
Aliyataja mashamba mengine kuwa ni Utumaini la Halmashauri ya Wilaya ya Mafia lenye ukubwa wa ekari 4,040 pamoja na shamba la Malonje katika Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga.
Waziri Lukuvi alisema bado kuna changamoto nyingi za mashamba ambayo wananchi wanataka umiliki wake ufutwe.
Kuhusu umilikaji wa ardhi, alikiri bado kuna tatizo katika maeneo mengi nchini ambayo licha ya viwanja kupimwa, bado halmashauri zinashindwa kuandaa michoro na hati za kuwapa wananchi wanaohitaji viwanja hivyo.
Akizungumzia Mji wa Kigamboni katika Jiji la Dar es Salaam, alisema wizara baada ya kuchunguza imeona kuna haja ya kupunguza eneo hilo baada ya marekebisho ya Tangazo la Serikali.
“Eneo la mpango limepunguzwa kwa kuondoa kata tatu za Mpiji, Pembamnazi na Kisarawe ambalo lina ukubwa wa hekta 44,440 ambazo hazikuwapo katika mpango wa awali, hivyo kubaki na kata sita zenye ukubwa wa hekta 6,494,” alisema Lukuvi.
Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, James Lembeli aliitaka Serikali kusimamia kauli yake kwamba haiwezekani kupima ardhi kama haijawalipa fidia wamiliki wa maeneo hayo.
Lembeli alisema mpango wa Serikali kutwaa ardhi ya wananchi bila kulipa fidia unatakiwa ukomeshwe na kutolewa maelekezo kwa taasisi zote kuacha kufanya uthamini utakaoidhinishwa na mthamini mkuu kabla halmashauri au mlipa fidia kuthibitisha kama ana fedha za kulipa.
“Kuna maeneo mengi ambayo wananchi wamechukuliwa maeneo yao bado hawajalipwa fidia.
“Ukiuliza tatizo nini, majibu yanakuja kuwa wanaopaswa kulipa fidia hawana fedha, huku ni kuwasumbua wananchi na pia ni kutafuta ugomvi usio wa lazima,” alisema Lembeli.

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!