Friday 5 December 2014

ZITTO: YANAYOENDELEA BIASHARA YA SUKARI NI ZAIDI YA ESCROW

Baada ya Watanzania kuliona Bunge likiwachukulia hatua vigogo waliohusika na ufisadi wa Akaunti ya Tegeta Escrow wa Sh306 bilioni, madudu mengine ya Serikali yanatarajiwa kubainika mara bada ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuanza kufuatilia sakata ya sukari nchini.

Hatua hiyo ya PAC kuanza kulifanyia kazi inatokana na malalamiko ya wamiliki wa viwanda vya sukari yanayotolewa kutokana na soko la ndani kutekwa na sukari inayoingizwa kutoka nje ya nchi na wafanyabiashara wakubwa.

Wiki iliyopita, Bunge lilifikia maazimio ya kutaka mamlaka za uteuzi ziwachukulie hatua kwa mujibu wa sheria, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospter Muhongo na katibu mkuu wa wizara hiyo, Eliakim Maswi, Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Frederick Werema kutokana na kuhusika kwao kwenye sakata la uchotwaji wa fedha hizo kwenye akaunti ya escrow na kupokea fedha hizo.

Mwenyekiti wa PAC, Zitto Kabwe anasema malalamiko na matatizo yaliyopo, watatumia kipindi cha mwezi huu na ujao kupitia suala la sukari kwa kuwa ni kubwa kuliko hata ufisadi uliojitokeza katika akaunti hiyo ya Tegeta Escrow.

“Hili suala la sukari ni kubwa kuliko hata la escrow kwani linagusa moja kwa moja maisha ya wananchi, wamiliki wa viwanda na uzalishaji na tayari tumeiita Bodi ya Sukari tujadiliane kwa kina kuhusu suala hili,” anasema Zitto.

Wamiliki wa viwanda Mkurugenzi wa viwanda vya sukari vya Kagera na Mtibwa, Seif Seif anasema hasara ambayo taifa litapata kutokana na kufungwa kwa viwanda hivyo ni kubwa kuliko serikali inavyofikiria.

Anasema jambo hilo linatokana na sukari inayozalishwa nchini- kwenye viwanda vyote vinne vya Kilombero, TPC, Kagera na Mtibwa- kuwa ni tani 320,000 huku mahitaji yakiwa ni tani 420,000.

Seif anasema kutokana na upungufu wa tani 100,000, walikubaliana na Serikali kwamba iwe inaagiza tani 100,000 ili kufidia upungufu huo, jambo ambalo linafanywa kinyume na makubaliano yao.
 “Leo hii ukipita katika maduka mbalimbali, utakunata na sukari ya kila aina huku sukari yetu ikiwa imesheheni katika maghala tukiwa hatujui wapi pa kuipeleka...na hao wanaoingiza sukari hiyo ni ushirikiano na vigogo wa serikali, jambo ambalo kwa sasa limeota mizizi na hatua za makusudi hazionekani.
“Tatizo hili linajulikana kuanzia ngazi za juu kabisa za uongozi kwani sio geni na kutokana na hali hiyo sisi wamiliki hatuoni sababu ya kuendeleza viwanda hivyo kwa hasara. Ni bora tuvifunge na tuangalie majukumu mengine ya kufanya,” anasema Seif.
Kutokana na ugumu wa biashara, Seif anasema wamepunguza wafanyakazi 2,000 na kubakiwa na 5,000 kwenye Kiwanda cha Kagera, Kilombelo 3,000 na wamebaki 6,000 na Mtibwa 3,000 wakikosa kazi kutoka wafanyakazi 6,000.
“Fikiria watu hawa ambao walikuwa wanafanya kazi katika viwanda hivi, wanakwenda wapi? Lakini hawa nao waliobaki tukivifunga watakwenda wapi? Hili ni swali ambalo Serikali inatakiwa kujiuliza baada ya sisi kufunga viwanda itawasaidiaje wananchi hawa ambao najua kabisa kwamba wana familia na wanategemewa?” anasema Seif.
Anasema uwekezaji wa sukari unahitaji uvumilivu kwani ili uanze kupata faida ni zaidi ya miaka 10 ukiwa hujapata kitu kutokana na maandalizi yake kuchukua muda mrefu hivyo serikali inatakiwa kuhakikisha inavilinda viwanda vya ndani ambavyo licha ya kuwekeza pia inasaidia katika huduma za jamii.
Mwenyekiti wa Bodi ya Kiwanda cha Sukari Kilombero, Ami Mpungwe anasema: “Hali ni mbaya, tunaona kuliko kuendelea na hali hii ni bora tufunge kuzalisha sukari kuliko kuendelea.
“Kama kweli Serikali ina dhamira ya kuvifufua na kuviendeleza viwanda vyetu vya ndani, ni lazima kuvilinda na kupiga marufuku uagizwaji holela wa sukari kutoka nje.”
Mpugwe anasema kufungwa kwa viwanda hivyo kutaathiri hata wakulima wadogo kwani watakosa sehemu ya kuuza miwa yao kwa kukosa soko, jambo ambalo pia litarudisha nyuma maendeleo ya wakulima hao.
Mipango ya Serikali
Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Mhandisi Christopher Chiza akisoma bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka 2014/15 alisema uzalishaji wa sukari kwenye viwanda vya Kilombero, Mtibwa, TPC na Kagera hadi 31 Machi mwaka huu ulikuwa tani 293,011, sawa na asilimia 99.91 ya malengo.
Anasema ongezeko hilo linatokana na sababu za kuwapo kwa mvua za kutosha, hususan katika maeneo ya Kilombero na Kagera; kupanua miundombinu ya kilimo cha umwagiliaji katika mashamba ya Kampuni ya Sukari Kagera; kutumia mbegu bora za miwa ambazo ni mpya aina ya N19 na N25 na ukarabati wa viwanda vya Kilombero na TPC.
Chiza alisema kumekuwapo na malalamiko ya wazalishaji wa sukari nchini kuhusu changamoto wanazokabiliana nazo, hususan ya kushindwa kuuza sukari katika soko la ndani kutokana na hisia kuwa kiasi kikubwa cha sukari kimeingizwa nchini bila kuidhinishwa na Serikali. “Kutokana na changamoto hiyo, wizara na wadau wa sukari waliazimia kuundwa kwa kikosi kazi kitakachotafiti na kutoa mapendekezo ya mfumo mzuri wa kuagiza sukari ambao hautaathiri uzalishaji wa ndani na upatikanaji wa sukari. Kikosi kazi kimeundwa na kinajumuisha wazalishaji wa sukari nchini, wakulima wa miwa, wataalamu wa sukuri, wawakilishi kutoka Wizara za Fedha, Viwanda na Biashara na Kilimo Chakula na Ushirika,” anasema Chiza.
Septemba mwaka 2011 Serikali ilipiga marufuku uuzaji wa sukari nje ya nchi, kufuta vibali vya kupeleka bidhaa hiyo nje pia ikitoa ofa ya kuiingiza kutoka nje bila kulipia ushuru.
Aliyekuwa katibu mkuu wa Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, Mohammed Muya alisema wakati akitoa agizo hilo kuwa mpango huo unalenga kupunguza bei ya sukari kwa rejareja na kukidhi mahitaji ya watumiaji.
Muya alisema kuwa serikali itakuwa inatoa vibali kwa wafanyabiashara wenye uwezo ili kuagiza sukari inayofikia tani 120,000 kutoka nje na kwamba mtu mmoja ataruhusiwa kuingiza shehena isiyozidi tani 5,000.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Uwekezaji na Uwezeshaji, Dk Mary Nagu, akifungua mkutano na wadau wa sukari uliofanyika mjini Morogoro Januari 11 mwaka huu, alisema: “Wadau wote kwa pamoja tuwe wawazi, wakweli na waaminifu kwa wale wote wanaotutegemea.”
Alisema ili kuondoa malalamiko ya mara kwa mara kwa wananchi kuhusu sukari, ni lazima viongozi wawe mstari wa mbele kulisimamia hasa wanapoona bei sukari inakuwa juu pasipo sababu ya msingi.
“Katika kusimamia bidhaa hii ya sukari inabidi tuchukue hatua ambazo zitafanya eneo hili kuwa endelevu na siyo hatua za muda mfupi zisizomaliza matatizo yaliyopo,” alisema.
CHANZO:MWANANCHI.

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!