Saturday 8 July 2017

BODI YA MIKOPO KUTANGAZA SIFA NA VIGEZO VITAKAVYOTUMIKA KUWAPANGIA WANAFUNZI MIKOPO 2017/2018


Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imesema hivi karibuni itatangaza sifa na vigezo vitakavyotumika kuwapangia wanafunzi mikopo ya elimu ya juu kwa mwaka wa masomo 2017/2018 unaotarajia kuanza miezi michache ijayo.



Ufafanuzi huo umetolewa jana (Ijumaa, Julai 7, 2017) jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Msaidizi wa Habari, Elimu na Mawasiliano wa HESLB, Dk Cosmas Mwaisobwa wakati akijibu maswali ya baadhi ya wateja waliotembelea Banda la HESLB katika Viwanja vya Mwalimu Nyerere ambako HESLB inashiriki katika Maonyesho ya 41 ya Kimataifa ya Biashara.


“Tunakamilisha mwongozo wa utoaji mikopo kwa mwaka ujao wa masomo na tumepanga kabla ya mwisho wa mwezi huu wa Julai tuwe tumeutangaza na tumefungua mtandao wetu ili waombaji wenye sifa waombe,” alisema Dk Mwaisobwa.


Dk Mwaisobwa amewataka waombaji wa mikopo watarajiwa wawe watulivu na kufuatilia kwa karibu vyombo vya habari na tovuti ya HESLB (www.heslb.go.tz) ambayo huwa na kiunganishi (link) cha mfumo wa kuombea mkopo.


Awali, katika maonesho hayo, baadhi ya wananchi wanaotarajia kuomba mikopo ya elimu ya juu wamepata fursa ya kuuliza maswali mbalimbali yakiwemo tarehe ambayo Bodi itaanza kupokea maombi ya mikopo kwa mwaka wa masomo 2017/2018.


Maswali mengine yaliyoulizwa ni kama utaratibu wa udahili kupitia vyuoni moja kwa moja utaathiri upatikanaji mikopo, wengine walitaka kupata elimu zaidi kuhusu taratibu za urejeshaji wa mikopo.


Akifafanua kuhusu maswali hayo, Dkt. Mwaisobwa alisema Sheria iliyoanzisha HESLB, pamoja na mambo mengine, inamtaka mnufaika kuanza kurejesha mkopo wake miezi 24 baada ya kuhitimu masomo.


Mkurugenzi huyo wa HESLB alisema kuwa sheria hiyo inamtaka mwajiri yeyote kuwasilisha kwa HESLB majina ya waajiriwa wake wote ambao ni wahitimu wa taasisi za elimu ya juu ndani ya siku 28 baada ya kuwaajiri na Bodi itamjulisha kama ni wanufaika au hapana pamoja na utaratibu na kiwango cha kumkata mnufaika. 



Dk Mwaisobwa aliwataka wananchi kutembelea banda la HESLB kwa kuwa Bodi ya Mikopo itaendelea kuonyesha shughuli zake kwenye banda lake lililopo ndani, Banda la Benjamin Mkapa (Namba 19&20) hadi mwisho wa maonyesho hayo, tarehe 13 Julai, 2017.

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!