Thursday 2 February 2017

Mvua yasababisha Mafuriko Mpwapwa, Watu zaidi ya wanne wapotea


16427263_1849402701984605_979886366526456850_n.jpg
Watu wanne wakiwamo watatu wa familia moja, wamefariki dunia baada ya nyumba zao kusombwa na mafuriko kutokana na mvua iliyonyesha usiku wa kuamkia jana katika Wilaya ya Mpwapwa mkoani Dodoma.



Hata hivyo, viongozi mbalimbali wametoa takwimu zinazotofautiana kuhusu idadi ya vifo vilivyotokea.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Jordan Rugimbana alisema watu wanane walikuwa wameripotiwa kufariki dunia na kuwa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa ilikuwa inajiandaa kwenda eneo la tukio ili kujionea uharibifu uliotokea.

Lakini, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Lazaro Mambosasa alisema taarifa alizonazo ni za watu watatu waliopoteza maisha na kwamba bado hajapata taarifa sahihi za tukio ambalo lilitokea katika vijiji vya Mang’angu na Chinyika katika Kata ya Ving’awe.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, mmoja wa manusura, Beka Mlami (10) alisema walikuwa wamelala wakiwa watano katika nyumba yao mvua kubwa ilipoanza kunyesha kuanzia saa tatu usiku na ilipofika usiku wa manane nyumba yao iliyojengwa kwa udongo ilisombwa na maji.

Mbali na yeye, wengine waliokuwa katika nyumba hiyo ni Martha Sumisumi (60), Shukuru Donald (15) aliyekuwa mwanafunzi wa kidato cha kwanza katika Shule ya Sekondari Mwanakianga, Bernadetha Sumisumi (9) aliyekuwa mwanafunzi wa darasa la kwanza katika Shule ya Msingi Ilolo na Joseph Sumisumi (12) ambaye alinusurika.

Beka alisema baada ya kuona maji yameingia ndani, aliwaambia ndugu zake wakimbie watoke nje na wakati wanajiandaa kuvaa nguo nyumba yao ilianguka na kuwaponda, lakini yeye alifanikiwa kutoka na kupanda juu ya bati.

Alisema baada ya kutoka nje ndipo gogo kubwa la mti lililosombwa na maji lilipopiga nyumba yao na kuanguka chini hivyo ndugu zake wengine kushindwa kutoka na hivyo kusombwa na maji.

Alisema baada ya kutoka nje alimwona ndugu yake mwingine Joseph akiwa anapelekwa na maji, lakini alifanikiwa kujiokoa.

Mkazi mwingine wa eneo hilo, Steven Noel alisema nyumba iliyosombwa na maji ilikuwa imejengwa karibu na korongo la maji, hivyo baada ya mvua kunyesha, maji yaliacha mkondo wake na kuingia kwenye makazi ya watu na kusababisha maafa hayo.

“Mvua ilisababisha mafuriko makubwa ambayo yalikuwa yamebeba na magogo makubwa ambayo yaliipiga ile nyumba na kuivunja katikati,” alisema Noel.

Alisema baada ya gogo la mti kuipiga nyumba hiyo, maji yalijaa ndani na kwa kuwa milango ilikuwa imefungwa, yalikosa njia ya kutokea na kuiangusha.

Noel alisema kulipopambazuka, walifukua na kuipata miili ya watu hao watatu huku mwili mwingine wa Jesca Lubeleje (19) mkazi wa Kijiji cha Chinyika ukiokotwa.

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!