Thursday 8 December 2016

Sita waokotwa mtoni ndani ya viroba

MAITI sita ambazo hazijatambulika zimekutwa zikielea katika Mto Ruvu eneo la Bagamoyo, Mkoa wa Pwani zikiwa zimehifadhiwa kwenye mifuko ya sandarusi maarufu viroba vya uzito wa kilogramu 200, huku zikiwa zimeharibika vibaya.


Akizungumza na gazeti hili kwa simu jana, Diwani wa Kata ya Makurunge, Paul Kabile alisema maiti hizo ambazo ni za jinsia ya kiume ziligunduliwa na wavuvi.
Kabile alisema maiti tano ziligunduliwa Desemba 6, majira ya alfajiri kwenye Kitongoji cha Kitopeni wilayani Bagamoyo, ambako wavuvi hao waligundua miili hiyo wakati wakiendelea na shughuli zao za uvuvi kwenye mto huo.
“Maiti hizo kila moja ilikuwa imehifadhiwa kwenye kiroba huku zikiwa zimewekewa mawe na mifuko hiyo ikiwa imeshonwa juu kama vile yamehifadhiwa mahindi au mchele,” alieleza Kabile na kuongeza kuwa wavuvi hao baada ya kuziona maiti hizo walizizika kutokana na kuharibika sana na kushindwa kuzipeleka hospitali kuzihifadhi.
“Wavuvi hao walizizika maiti hizo huku kukiwa hakuna taarifa yoyote juu ya kuwa zimetokea wapi na ni watu gani waliofanya tukio hilo,” alisema Kabile na kubainisha kuwa maiti nyingine moja iligundulika jana.
Mwandishi wa Habari wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani, Hassan Mtengevu alithibitisha kutokea tukio hilo, na kueleza kuwa wanafanya uchunguzi kwa kushirikiana na daktari ili kufahamu watu hao walikufa kwenye mazingira gani.

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!