Saturday 12 November 2016

Mbaroni kwa kunajisi mtoto wa miaka 3


Image result for justice
MVUVI katika kijiji cha Utinta kilichopo mwambao mwa Ziwa Tanganyika wilaya ya Nkasi mkoani Rukwa, James Kibwe (58) amefikishwa mahakamani kwa kosa la kumnajisi mtoto wa jirani yake mwenye umri wa miaka mitatu.

Mshtakiwa huyo amefikishwa mbele ya Hakimu Mkazi wa Wilaya ya Nkasi, Ramadhani Rugamalila na kusomewa mashtaka ambayo aliyakana.
Mwendesha Mashtaka, Mkaguzi wa Polisi, Hamimu Gwelo alidai mahakamani hapo kuwa mshitakiwa huyo alitenda kosa hilo, Novemba 11 mwaka huu, saa tisa mchana kijijini Utinta.
Gwelo alidai siku hiyo ya tukio, mshtakiwa alimhadaa mtoto huyo kuwa atampatia pipi ambapo aliongozana naye hadi nyumbani kwake, ambako anadaiwa kumfanyia unyama huo na kumsababishia maumivu makali kwenye sehemu zake za siri.
Ilidaiwa mahakamani hapo kuwa, mtoto huyo aliporejea nyumbani, mama yake mzazi alimwona akitembea huku akichechemea ndipo alipomkagua na kugundua, alijeruhiwa sehemu za siri.
Gwelo alieleza kwamba, majirani walimueleza mama huyo kuwa, walimuona binti yake huyo mdogo akiongozana na mshtakiwa na kuingia nyumbani kwake ambako mshitakiwa huyo anaishi.
Mshtakiwa huyo amerudishwa rumande, huku shauri lake likiahirishwa hadi Novemba 23, mwaka huu baada ya kushindwa masharti ya dhamana yaliyomtaka awe na wadhamini wawili kila mmoja akiwa na mali isiyohamishika yenye thamani ya Sh milioni mbili.

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!