Tuesday 9 February 2016

MARADHI YA ZIKA YALIANZA AFRIKA MASHARIKI MIAKA 58 ILIYOPITA


Hivi sasa duniani kote kuna hofu ya kuwepo homa itokanayo na virusi vya Zika, vinavyosambazwa na mbu.

Katika nchi mbalimbali, ikiwemo Marekani ambako kuna hofu kubwa ya kusambaa homa hiyo kuna jitihada kubwa za kujihami kitaalam zinafanyika.
Wataalam watafiti wanaeleza kuwa, ni janga lenye historia ya tangu miaka ya 1950, asili yake iko kwenye baadhi ya maeneo ya bara Afrika na Asia.
Nchini Tanzania ambako juzi kupitia vyombo vya habari, serikali iliripoti bado kuko shwari dhidi ya maradhi hayo, historia yake inaonyesha kuna ‘nyayo’ zake katika ugonjwa huo ambao mzizi wake ni Afrika Mashariki muda mrefu uliopita.
Mwaka 2014 iligundulika kasi ya kusambaa maradhi hayo katika maeneo mengi ya Ufaransa, Marekani ya Kusini, visiwa vya Caribbean na Mexico.  
Juzi vyombo vya habari viliripoti taarifa ya serikali kwamba, homa ya Zika haijafika nchini na wananchi wasiwe na shaka nayo.        
DALILI NA TIBA
Inaelezwa, katika wastani wa kitabibu katika maeneo ambako kuna athari, ni kwamba kati ya watu watano walioambukizwa, mmoja ndiye anaonekana katika hali ya kuumwa.
Dalili zake ni pamoja na kupata homa, maumivu ya viungo na kuwa na macho mekundu. 
Hata hivyo, kipindi cha mahsusi cha kutambua mtu alipoambukizwa hadi dalili kuanza kuonekana hazipo bayana, ingawaje inakadiriwa ni chini ya wiki moja ndio mtu huumwa kwa kipindi kinachokadiriwa cha wiki moja.
Virusi vya Zika hukaa katika damu ya mwilini mwa mtu na dalili zake zinaelezwa kufanana sana na homa ya dengue.
Haina tiba rasmi wala chanjo, ingawaje inalezwa kuwa haina matukio mengi ya vifo.
Mgonjwa anayesumbuliwa na maradhi hayo anashauri kuwa, katika kipindi hicho awe na mapumziko ya kutosha na kunywa maji mengi, ili kuzuia maji yanayopotea mwilini kutokana na kuugua huko.
Kama ilivyo kwa dengue, wakati wa kuugua zika inaelezwa kuwa si sahihi kutumia dawa jamii ya aspirini, kwani zinakuwa na athari kwa mgonjwa na ni vyema kuepuka mbu kwa kiasi kikubwa.
Wataalam wanasema kuwa, kuna uwezekano wa maambukizi ya homa ya Zika, kutoka kwa mama aliyeambukizwa hadi kwa mtoto.
HARAKATI ZA MAREKANI
Kuanzia mwezi uliopita, Kituo cha Kuzuia Maradhi cha Marekani, ilitoa miongozo ya kiafya kwa wasafiri katika ya nchi hiyo na zile zilizoathirika na maradhi hayo na kinamama wajawazito, ikiwezekana waahirishe safari zao.           
Serikali zinginezo duniani zimeanza kuchukua harua kama hizo. Baadhi ya nchi hizo ni Colombia, Jamhuri ya Dominica, Ecuador, El Salvador, na Jamaica.
CHIMBUKO LA ZIKA 
Watafiti wa masuala ya homa ya njano, wanasema Maradhi ya Zika yalianza kuonekana rasmi mwaka 1947, kutoka kwa nyani waliokuwepo misituni nchini Uganda.
Hatua ya pili kugundulika ilikuwa Januari mwaka 1948 na hadi kufikia mwaka 1952, iligundulika rasmi na kupewa jina la ‘homa ya Zika’ ikiwa mwilini kwa nyani. 
Lakini ilipofika mwaka 1968, iligundulika mwilini mwa binadamu nchini Nigeria. Hapo ndipo kukawepo mwendelezo wa simulizi za kugundulika katika nchi zingine wanadamu wakiambukizwa, kati ya mwaka 1951 na 1981.
Kuna ushahidi unaoeleza kuwa katika nchi za Kiafrika kama vile Tanzania, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Misri, Gabon, Sierra Leone na Uganda.
Vivyo hivyo na mataifa ya India, Indonesia, Malaysia na Philippines, Thailand na Vietnam, sasa ikitijkisa katika maeneo kama ya French Polynesia.
Kabla ya hali iliyoko sada kuhisiana na maradhi hayo, kwa maana ya mwaka 2007, homa ya Zika haikuwa na kasi kubwa ya kusamba akama inavyoonekana sasa.
 KWA NINI INASAMBAA SANA?
Inaelezwa kuwapo safari nyingi za kibiashara zina mchango mkubwa wa kuisamba akwa homa ya Zika. 
Sasa inaelezwa, kasi ya kusambaa inatia shaka, hasa pale ilipovuka mabara kadhaa na kutua Ulaya na Marekani, hata ikaweka rekodi ya kipekee ya kusafiri mbali zaidi duniani.
Marekani katika utafiti mmojawapo iligundua mbu wanaelezwa kuwa na uwezo wa kubeba virusi vya Zika, walipatikana katika eneo moja la milima, jirani na jiji la Washington D.C na wanaweza kuishi kulingana na mabadiliko ya hali ya hewa duniani.
Ripoti ya Umoja wa Mashirika ya Afya ya Marekani (PAHO), imebaini kusambaa kwa homa ya Zika katika nchi jirani kama vile Barbados, Bolivia, Brazil na Colombia.
Nyingine ni Jamhuri ya Dominica, Ecuador, El Salvador, Guadeloupe, Guatemala, Guyana, visiwa vya Haiti, Honduras, Martinique, Mexico, Panama, Paraguay, Puerto Rico, Saint Martin, Suriname na Venezuela.
KUAMBUKIZA KWA KUJAMIIANA
Mwaka 2009, mtaalam wa bailojia kutoka Chuo Kikuu cha Jimbo la Colorado, alimuambukiza homa ya Zika mke wake kwa njia ya kujamiiana, baada ya kutoka katika eneo lenye mbu wengi wanaoambukiza Zika.
Hiyo ilikuwa baada ya kusafiri kutoka nchini Senegal, kufanya uchunguzi wa karibu kuhusu mbu wasambazao homa hiyo na ndipo alipofanya mapenzi na mkewe.
Kipindi kifupi baadaye, mtu huyo akaanza kuonyesha dalili za mgonjwa wa Zika. Katika taarifa rasmi za kitaalam, Foy anakuwa mtu wa kwanza kumuambukiza mkewe virusi vya maradhi hayo kwa njia hiyo.

No comments:

 

ADVERTISE WITH US

AFRICAN FASHION

PLACE YOUR ADS HERE!